Saturday, June 2, 2012

Elimu ya sanaa irudishwe tena mashuleni kuanzia shule za awali


Wanafunzi waliohitimu Alphabeta Music Centre, Tabata
Asilimia kubwa ya wanamuziki hapa Tanzania wanapiga muziki bila ya kuwa na elimu yoyote ya awali ya muziki. Viongozi wengi wa nchi wamekuwa wakitoa kauli nzuri za kusifu sanaa hii na wasanii wa sanaa hii lakini ni nadra kusikia kiongozi akiongelea matayarisho rasmi katika sanaa hii, na kwa ukweli hata katika sanaa nyingine.
Kama ambavyo kumekuweko na kufa kwa viwanda nchini humu ndivyo ilivyotokea katika elimu ya sanaa. Zamani sanaa ilianza kufundishwa kuanzia darasa la kwanza, na hata syllabus ya elimu hiyo mpaka leo ipo, ila haitumiki. Vyuo, kama Chuo cha Waalimu Butimba kule Mwanza, kilitoa waalimu ambao walikuwa maalumu kwa ajili ya kufundisha sanaa katika shule zetu kuanzia shule za msingi, bahati mbaya sana haya yote yametupwa uvunguni, hivyo Taifa linakwenda kihobelahobela katika tasnia ya sanaa. Kuna vyuo, kwa mfano Chuo cha Sanaa Bagamoyo, ambacho hupokea wanafunzi kwa ajili ya kupata elimu ya sanaa, lakini utaona wazi kwa kuwa hakuna mtiririko wa elimu hiyo kutokea shule za msingi, elimu hiyo ina walakini. Na zaidi katika ngazi ya Chuo Kikuu, mtu anapata digrii baada ya kusoma miaka mitatu  bila ya kuwa na elimu ya awali inayoonyesha mtu huyu alikuwa na vyeti gani vya msingi katika taaluma yake.
Utafiti umeonyesha kuwa kupata elimu ya muziki kuanzia umri mdogo kuna faida nyingi sana. Kwanza humuwezesha mtoto kukuza sehemu ya ubongo ambayo huhusika na lugha na pia kukuza uwezo wake wa kutafakari. Inaeleweka kuwa ubongo huendelea kupata maendeleo miaka mingi baada ya kuzaliwa, hivyo muziki huendeleza kuboresha upande wa kushoto wa ubongo ambao ndio huhusika na ujuzi wa lugha na  tafakari. Muziki husaidia sana watoto kukumbuka mambo mbalimbali, ndio maana hata matangazo ya biashara ya kawaida husindikizwa na muziki ili kukaa katika kumbukumbu kwa urahisi. Kwa watoto, muziki husaidia sana katika kazi zao za elimu ya kila siku.
Wasanii waliopata elimu sahihi huwa na uwezo wa kubuni majibu mbali mbali kwa tatizo moja, hii unaweza kuiona kwa mfano ukiwapa wanamuziki kumi semina kuhusu jambo, kwa mfano ukimwi kisha ukawambia watunge wimbo kuhusu elimu waliyopewa, utashangaa watakuja na tungo tofauti za mtizamo mpya kabisa wa kuelezea elimu hiyo waliyoipata. Elimu ya muziki  hufungua ubongo  kuruhusu kuachana na mawazo mengi yaliyopita na kujaribu mawazo mapya. Wasanii kote duniani huwa waanzilishi wa mambo mengi ikiwemo mitindo ya nguo, uvaaji na mambo mengi katika maisha kutokana na ubongo wao kuwa na uwezo wa kuruhusu kufikiria vitu katika mtazamo mpya. Elimu ya awali ya muziki imeonyesha kuwa wanafunzi wa elimu hii hufanya vizuri zaidi katika masomo mengine, tofauti sana na mawazo ya kawaida kuwa muziki huharibu watoto. Katika muziki, kosa huwa ni kosa , ukikosea beat, usipotyuni chombo chako, ukiimba vibaya ni kosa hakuna mbadala, sauti ikiwa juu mno, au chini mno nakadhalika, na mwananmuziki hulazimika kurudia tena na tena mpaka atakapopata kitu sahihi kabisa, elimu hii ikiwa kichwani kwa mtoto toka umri mdogo humsaidia katika kuboresha mambo yake mengine na kuyafanya vizuri zaidi kila mara. Elimu ya awali ya muziki humjenga mtoto kujua kufanya kazi na watu wengine kama kundi, kutokana na kuelewa kuwa katika muziki watu wengi hutegemeana ili kuleta ubora katika wimbo mmoja, hii huwasaidia katika maisha ya kila siku. Kuna mengi yanayopatikana katika elimu bora ya sanaa, pia kubwa likiwa ni kwenda sambamba kitaaluma na ulimwengu, kuna bahati mbaya sana kwa vijana wetu kutaka kuingia katika soko la muziki duniani lakini bila kuwa na matayarisho yanayostahili kufikia huko, wengi ndoto zao hazitatimia kwani elimu ya kufikia huko hawana.

Sunday, May 27, 2012

Meneja wa African Stars Band afukuzwa kazi


Martin Sospeter (kushoto)
Mkurugenzi wa African Stars Asha Baraka ametangaza kumfukuza kazi  Meneja wa Bendi ya African Stars Band bwana Martin Sospeter. Kati ya sababu ambazo zimepelekea Meneja huyo kuchukuliwa hatua hiyo ni pamoja na kinachodaiwa kuwa na mipango ya kushawishi wanamuziki wa bendi hiyo kuhamia bendi nyingine mjini ya Mashujaa Muzika

Friday, May 25, 2012

Maafisa Utamaduni unajua kuwa hawako chini ya Wizara ya Utamaduni?


Pamoja na maelezo mazuri ya Serikali kuwa inawajali wasanii, kuna maswali kadhaa ambayo yanajitokeza na kuleta maswali makubwa zaidi. Idara ya Utamaduni imekwisha hama Wizara zaidi ya kumi toka nchi hii ilipopata Uhuru, kwanini?,  Mwaka 1995 na pia mwaka 2010,Idara hii ilisahauliwa kutajwa wakati wa kutangaza Baraza la Mawaziri baada ya Uchaguzi Mkuu, mwaka 2010 tulipewa taarifa kuwa jambo hilo lilitokea kwa bahati mbaya mwaka 1995 hapakutolewa maelezo yoyote, ila kimya kimya ikaelezwa Utamaduni utaendelea kuwa chini ya Wizara ya Elimu.
Kuanzia kipindi cha miaka ya 90, Serikali ilifuta ngazi kadhaa za uongozi katika  Utamaduni, kulikuweko na nafasi ya Kamishna wa Utamaduni haiko tena, kulikuweko na nafasi ya  Afisa Utamaduni Mkoa, nayo haiko tena. Wako Maafisa Utamaduni wa Wilaya na Manispaa, lakini hawa sasa wako chini ya TAMISEMI, Wizara tofauti na ile inayohusika na Utamaduni. Haichukui akili kubwa kuona tatizo lililo wazi linatokea.
Nimeshawahi kumsikia Afisa Utamaduni mmoja Jijini Dar es Salaam akitamba kuwa yeye hababaishwi na Baraza la sanaa La Taifa, na ni kweli kwani hayuko chini ya Wizara ya Utamaduni.
Shughuli za pamoja za Kitaifa zilnazohusu Utamaduni ni ngumu kuzifanya sasa, Mashindano ya Kitaifa ya kazi za sanaa hayasikiki tena, pia hata shughuli zinazohusika na maslahi ya pamoja ya wasanii kama vile ulinzi wa haki za wasanii kwa mfano Hakimiliki umekuwa hobela hobela maana hakuna ajenda ya pamoja kwa viongozi hawa wanaotegemewa kuwa karibu kabisa na wasanii. Maafisa Utamaduni wa Wilaya wamekuwa zaidi ni wakusanyaji wa pato la Wilaya bila kuwa na mchango kwa wadau waliomo katika tasnia mbalimbali za Utamaduni wilayani mwao. Miaka ya nyuma sana Afisa Utamaduni alikuwa kimbilio la msanii, aliweza kutafuta vifaa vya muziki kwa wanamuziki, kutafuta maeneo ya kufanyia mazoezi kwa wasanii wasio na nafasi. Community Centers zilikuwa chini ya Afisa Utamaduni na kuwa mahala ambapo pako chini ya serikali na maalumu kwa shughuli za sanaa. Community Centers hazipo tena baada ya kugeuzwa aidha ofisi za Manisipaa au kukodishwa kwa watu binafsi kuongeza pato la serikali za mitaa bila kujali vijana waliomo katika Manispaa wanapewa sehemu maalumu kufanya shuguli zao za sanaa.
Ukiangalia Bajeti ya TAMISEMI  unajiuliza ni asilimia ngapi ya bajeti hiyo ilienda katika shughuli za Utamaduni? Utamaduni ukilelewa vizuri ni chombo chenye nafasi nyingi sana za ajira, huweza kuongeza pato la eneo husika kwa kuhamasisha maendeleo, kuleta uzalendo, ubunifu wa mambo mbalimbali ya Utamaduni huweza kuhamasisha Utalii katika Utamaduni, sehemu ya Utalii ambayo kwa bahati mbaya sana haijatumika kikamilifu katika kuongeza kipato cha nchi hii kwa ujumla.
Si ajabu siku hizi kusikia wasanii wakisema tutaenda kumuona Rais atusaide katika hili au lile, ni jambo la kusikitisha kuwa matatizo ya wasanii dawa mpaka kumuona Rais, wasanii wangapi wanaweza kupata nafasi hiyo katika nchi hii yenye watu milioni zaidi ya 40?
Ni muhimu kuangalia upya mfumo huu wa utawala katika nyanja ya Utamaduni

Ngoma Africa Band kutumbuiza katika sherehe ya siku ya taifa ya Cameroon


Bendi maarufu ya muziki wa dansi barani ulaya "Ngoma Africa Band" aka FFU, inatarajiwa kupanda jukwaani kesho Jumamosi tarehe 26 May, mjini Stuttgart,Ujerumani kutumbuiza
katika sherehe ya siku ya taifa la Cameroon. Ngoma Africa Band watakuwa katika ukumbi wa Arena la  Sportpark Feuerbach, uliopo mtaa 
(Triebweg 85, 70469 Stuttgart) ,Wakamerooni wapatao 5,000 wanaoishi ujerumani pamoja
na maelfu ya wapenzi wa muziki nchini Ujeruamani wanategemewa watajimwaga uwanjani kupata burudani
kamili. Ngoma Africa sasa wanatamba na wimbo mpya "Uhuru wa Habari" ambao unasikika at
https://mail.google.com/mail/images/cleardot.gif



Tuesday, May 22, 2012

John Mbula anaumwa anahitaji msaada

Baadhi ya wanamuziki wa awamu mojawapo ya Atomic Jazz
Nimepata waraka huu kutoka kwa mwanamuziki mkongwe Benno Villa Anthony...................................Mkuu, kwanza kabisa namwomba Mwenyezi Mungu akujalie roho ya uvumilivu ktk kufuatilia taarifa hii. Itakumbukwa kuwa mwanzoni mwa mwaka huu, nilikuwa na kipindi cha mahojiano na Manju wa muziki na mtangazaji wa TBC,  komredi Masuud Masuud. Kwa vile kipindi kilirudiwarudiwa na huku Manju akitamka namba yangu ya simu, wengi waliinukuu,  na kati ya hao walioinyaka ni Mzee John Mbulla, aliyekuwa mpiga sax wa Atomic Jazz. Mzee huyu kwa sasa kweli anaumwa sana. Zaidi ni maradhi ya macho, haoni. Kumbe kwao ni Mpwapwa ila kwa sasa anahifadhiwa na diwani wa Kibaigwa, Ndugu Richard Kapinye.......0717  303070. Baada ya kusikia kuwa wasanii wanachangiana ili kupata tiba, Diwani huyo alinipigia na nikazungumza nao wote wawili. Wameniomba nikupe taarifa hii ili uitoe kwenye vyombo vya habari, ikiwezekana apate msaada wa tiba. Diwani anasema kuwa John akipata operation ya macho atapona na kuanza kujitegemea maana nguvu bado anazo. KUMBUKA...Mzee John Mbulla ndiye aliyepiga Saxaphone kwenye wimbo wa "TANZANIA YETU NDIYO NCHI YA KUSIFIWA", wakati Mbaraka Mweshehe alipojiunga na Atomic Jazz  kwa muda..............Mkuu Kitime, Nina uhakika kama wana Media wakimtembelea na kutoa habari zake, naamini wengi wataguswa na kumsaidia.  Natanguliza shukrani zangu za awali. Asante Mkuu. 

Monday, May 21, 2012

Robin Gibb wa BeeGees afariki dunia kwa kansa ya tumbo


The BEE GEES
Robin Hugh Gibb, mwanamuziki wa kundi maarufu la BEE GEES amefariki. Robin  alizaliwa tarehe  22 Desemba mwaka 1949.  Kundi la Bee Gees lilianzishwa kwa pamoja na pacha wake Maurice na kaka yao Barry japo Robin ndie aliyejulikana zaidi katika kundi hili. Wazazi wao walikuwa Waingereza japo kwa kipindi fulani walihamia Australia. Inasemekana kundi hili ndilo lililokuwa na mafanikio kuliko kundi lolote jingine la Pop duniani. Kwa karibu miongo 6 kundi hili limekuwa jukwaani. Kundi liliweza kuuza zaidi ya santuri milioni 200.

 Watanzania wengi walianza kuwafahamu baada ya kusikia vibao vyao kama Staying Alive, Night Fever, How deep is your love na kadhalika  katika filamu ya filamu ya Saturday Night Fever. 

Tarehe 20 May 2012 Robin amefariki baada ya matatizo ya muda mrefu ya kansa ya utumbo. Pacha wake Maurice alifariki kwa tatizo hilohilo 2003.

Grammy Awards za BeeGees

1977 Best Performance by a Group — "How Deep Is Your Love"
1978 Best Performance by a Group — "Night Fever"
1978 Album of the Year — "Saturday Night Fever"
1978 Producer of the Year — "Saturday Night Fever"

1978 Best Arrangement of Voices — "Stayin' Alive"
2000 Lifetime Achievement Award
2003 Legend Award