Wednesday, June 19, 2013

MAONYESHO YA LADYJD NA MWANAFA WANAMUZIKI WAMEJIFUNZA NINI?

Kuna somo ambalo liko wazi kabisa. Vikundi vyetu vingi hufanya hata zaidi ya maonyesho matano kwa wiki, na kupata mapato kiduchu, mara nyingine hata fedha ya usafiri kuwarudisha wanamuziki nyumbani baada ya onyesho haipatikani. Lakini tumeona kuwa maonyesho haya makubwa yaliyopangwa na kutayarishwa vizuri na pia kupewa promo ya kutosha huweza kuingiza kipato katika siku moja ambacho ni sawa na mapato ya miezi kadhaa ya vikundi vyetu katika mtindo wa sasa wa maonyesho ya kila siku yasiyo na matayarisho ya kutosha. Wanamuziki tutafakari!!!!!!!!!!!!!!

Tuesday, June 18, 2013

SAIDA KAROLI ASEMA SINA MPANGO WA KUFA BADO

SAIDA VERY
-->
Baada ya taarifa kuzushwa kuwa Saida Karoli amefariki katika ajali ya meli habari za uhakika ni kuwa Saida Karoli wala hayuko mahala popote jirani na Ziwa  Victoria. Baada ya kuweko Dar es Salaam wiki iliyopita, Saida na kundi lake walikodishwa na kuelekea Makongorosi Chunya mahala aliko mpaka asubuhi hii. Saida Karoli anasema hana mpango wowote wa kufa KARIBUNI. 
MUNGU AMUONGEZEE SIKU NYINGI ZENYE FARAJA KATIKA MAISHA YAKE

HABARI ZIMEENEA KUWA INAHOFIWA SAIDA KAROLI AMEFARIKI DUNIA

Kutokana na maelezo kutoka blog mbalimbali ikiwemo Mjengwa Blog na Sundayshomary.com mwanadada muimbaji aliyekuwa kipenzi cha Watanzania mara baada ya kutoa wimbo wake Chambua kama karanga, Bi Saida Karoli amefariki dunia baada ya chombo alichokuwa akisafiria kutoka kisiwa cha Goziba kuzama baada ya kupigwa na dhoruba kubwa. Bado habari zaidi hazijapatikana hivyo tunasubiri habari za ziada na kuweza kuwapasha wapenzi wa mwanadada huyu.

Thursday, June 13, 2013

LANGA KILEWO AFARIKI DUNIA

Msanii mwingine wa Hiphop Langa Kilewo ayelianza kujulikana katika kundi la Wakilisha akiwa na Witness na Shaa amefariki dunia mchana huu. Taarifa za Langa kuwa amelazwa hospitali zilianza kujulikana mapema leo katika blog kadhaa zenye kufuatilia wasanii, zikieleza kuwa kalazwa kwa tatizo la malaria. Langa ambae aliwahi kukiri hadharani kuwa ana tatizo kubwa la madawa ya kulevya na kutangaza kuwa ameachana na madawa hayo kutokana na matatizo yaliyokuwa yanamletea. Hivi  karibuni kama wiki mbili zilizopita, Langa  alikuwa akihojiwa katika kipindi cha Friday Night Live cha EATV akawa akimuongelea marehemu Ngwear na kumsifu sana kuwa alikuwa na roho safi, pia Langa alikuwa anaelezea mipango yake ya baadae baada ya kutoa video yake mpya aliyoifanya na P Funk na Fid Q iliyokuwa ikiitwa Rafiki wa kweli. Alikuwa akiongelea kukamilisha video zake nyingine mbili ili kutoa album mwishoni mwa mwaka. Hayatakuwa.
MUNGU AMLAZE LANGA KILEWO PEMA PEPONI