RAIS WA BURUNDI ATOA TAMKO KUPIGA MARUFUKU WANAWAKE KUPIGA NGOMA

RAIS  wa Burundi Pierre Nkurunziza, ametoa agizo jipya kuhusu upigaji wa ngoma za matambiko na kupiga marufuku wanawake kupiga ngoma hizo. Pia ameamuru kuwa ngoma hizo za matambiko kupigwa tu katika shughuli maalumu. Katika agizo lake imeelezwa kuwa ni marufuku mwanamke kupiga ngoma hizo za tambiko lakini wanawake wanaruhusiwa kushiriki katika kucheza wakati wakipigiwa ngoma hizo.
Pia amri imetolewa kuwa vikundi vyovyote ambavyo vinataka kufanya maonyesho ya sanaa hiyo, lazima vijiandikishe Wizara ya Utamaduni na havitakuwa na ruksa kufanya maonyesho hayo katika shughuli zisizo rasmi.

Ngoma hii ya matambiko ya  Burundi, mwaka 2014 iliwekwa katika orodha ya mali asili za dunia na UNESCO na kuingizwa katika  UNESCO’s Intangible Cultural Heritage list, ambapo ngoma hii inaelezewa kuwa ni muunganiko wa ngoma na kucheza kukiambatana na mashahiri ya ushujaa, na pia nyimbo za kiasili za Burundi. Kama ilivyo katika nchi nyingi za Kiafrika  ngoma hii ya tambiko siku hizi inachezwa kama burudani, lakini kwa miongo mingi ilikuwa ni ngoma iliyoabudiwa na kabila zima la Kirundi. Katika siku za karibuni ngoma hii imekuwa ikichezwa kwenye maharusi, graduation hata ubatizo. Ngoma hii ambayo awali ilikuwa ikipigwa na wanaume tu, kwa sasa kulianzishwa hata vikundi vya wanawake ambavyo vilianza kupiga ngoma hii. Kwa tamko jipya kila anaetaka kufanya onyesho la ngoma hii atalipia $280, na kama onyesho litafanyika nje ya nchi kiwango hicho kitalipwa kila siku. 

Comments