UNATAKA KUANZISHA BENDI? SOMA HAPA


Unajiona una uwezo wa kuanzisha bendi, je uanzie wapi? Pengine nikueleze vitu ambavyo wanaoanzisha bendi wengi huanza kuviwaza na kuvipanga ambavyo ikiwa uko serious unataka kuanzisha bendi lazima uvikwepe kama ukoma.
1.  Usianzishe bendi ili kushindana na bendi fulani…..umekwisha kabla hujaanza
2.  Usianzishe bendi kwa kuwa fulani kaweza kuanzisha…umekwisha kabla ya kuanza
3.  Usianzishe bendi ili ipige kama kama Wenge au Franco…umekwisha kabla hujaanza
4.  Usianzishe bendi ukategemea kuwa kwa kuloga bendi itakuwa juu….umekwisha kabla ya kuanza
Bendi yenye uwezekano wa kuendelea huwa ni bendi iliyoanzishwa na wanamuziki, ambao wanakuwa na aina ya muziki au ndoto ya muziki wanaotaka kupiga. Mara nyingine ndoto hii anaweza kuwa nayo mwanamuziki mmoja tu, akiwa anajua kabisa anataka kupiga muziki wa aina gani atatumia vyombo gani, ataendesha mazoezi vipi, uwezekano  wa kuendelea ni mkubwa zaidi. Na kama ilivyo miradi mingine ni muhimu anaeanzisha bendi awe na maono ya wapi atakuwa katika miezi mitatu, sita mwaka, miaka miwili, mitano na kadhalika. Bendi inayokwenda bila kujua inakwenda wapi hata inapoanza kuangula huwa haijijui kama imeanza kuanguka. Mpaka hapo utaona sishauri asie mwanamuziki kuanza mipango ya kuanzisha bendi, kazi hiyo waachie wanamuziki.  Ikiwa unataka kufanya biashara ya muziki nawe si mwanamuziki angalia nafasi yako katika hili, ingia katika makubaliano na wanamuziki ili wakulipe kiwango fulani, au asilimia fulani  kwa kila onyesho au kila wiki au kila mwezi kama vile wafanyavyo wenye magari ya kukodi,hili litakuondolea kichwa kuuma kuwaza utapata wapi mishahara kodi za nyumba na kadhalika. Najua hili ni gumu kwani kale kamvuto kakutambulika kama wewe ndie mwenye bendi kagumu kukakwepa. Kuna watu huingia katika mtego wa kuanzisha bendi na kupata fedha nzuri wakati wa uchanga wa bendi, baada ya muda wao ndio kazi yao kubwa inakuwa ni kutoa ruzuku kwa bendi, kwani kuiacha bendi ife inakuwa ngumu. Ushauri mzuri ni kutokuhangaika kudhibiti fedha za mlangoni bali kukodisha vyombo au kuingia mkataba wa malipo ya kiwango fulani kwa maonyesho na wanamuziki, wangapi wenye daladala hukaa kufuatilia konda kakusanya shilingi ngapi? Ni kupoteza muda kufanya kazi ambazo zina wenyewe. Na mara nyingi utajikuta unamuweka ndugu achunge kipato, nah ii mara nyingi nimekuta inaleta matatizo kwani ndugu hawa huwa hawajui mwanzo wa hadithi na hata umuhimu wa wanamuziki na huamini kuwa bendi ni vyombo, na kuingia katika uhasama mkubwa na wanamuziki ambao hupelekea kufa kwa bendi……………

Comments

Anonymous said…
Nakubaliana nawe.