UPANGA ILIWAHI KUITWA SOULVILLE


KATIKA  miaka ya 60 na 70 mpaka 80, karibu kila eneo la jiji la Dar es Salaam kulikuwa na makundi ya muziki. Wakati huo muziki ulifanywa kwa makundi tofauti na sasa ambapo msanii anaweza kuwa peke yake  katika kutunga, kurekodi na hata kufanya kazi yake jukwaani.  Muziki wa dansi uligawanyika katika makundi makubwa mawili, makundi yaliyopiga muziki wa rhumba na yale yaliyopiga muziki wa magharibi. Kulikuwa na ushindani mkubwa sana kati ya makundi haya kila mtaa ukijitahidi  kupiga muziki bora zaidi ya mwingine. Hata wazazi nao walijihusisha kuchangia ufanisi wa vikundi vya watoto wao, kwa kuwanunulia vyombo vya muziki na kuwapa maeneo ya kufanyia mazoezi. Kulikuwa na ushindani mkubwa sana kati ya vikundi vya muziki kutoka Kurasini na Chang’ombe na vikundi ambavyo vilitoka Upanga. Ukiliangalia eneo la Upanga leo huwezi kudhani kuwa lilikuwa eneo muhimu sana katika shughuli za muziki wa vijana, lakini hakika eneo hili lilikuwa na vikundi kadhaa vilivyokuwa na wanamuziki kutoka ambao wengi walikuwa ni watoto wa Upanga na wenzao ambao walijiunga nao wakitoka mitaa mingine. Upanga ni eneo muhimu sana katika historia ya muziki Tanzania. Enzi hizo vijana walipagawa na muziki wa soul, muziki ambao asili yake ilikuwa Marekani, muziki ambao uliporomoshwa na wanamuziki kama Otis Redding, Percy Sledge, Sam Cooke, James Brown, Clarence Carter, Wilson Pickett, Aretha Franklin na wengi wengine. Vikundi vingi vya muziki vya vijana wa Upanga, waliiga na kupiga muziki huu, na hata kuamua kupaita upanga, Soulville.

Kwenye kona ya barabara ya Mindu na United Nations, nyumbani kwa familia ya Jengo, hapo ndipo palikuwa mahala pa mazoezi pa kundi moja maarufu lililoitwa Groove Makers. Baadhi ya wanamuziki wa kundi hili walikuwa Mohamed Maharage, Joseph Jengo na nduguye Emmanuel Jengo, Herbert Lukindo, Willy Makame, na mpiga Drums ambae mpaka leo yupo katika anga za muziki Habib Jeff mwanamuziki ambaye toka amejiunga Mlimani Park miaka ya 70 hajawahi kuhama kundi hilo. Kundi jingine maarufu pale Upanga lilikuwa The Strokers, hili lilikuwa na awamu mbili, awamu ya kwanza ilikuwa na wanamuziki akina Donald Max, David Max, Harry Chopeta, Vincet Chopeta, Pino Makame na Ochiwa na Freddy Lukindo.

Awamu ya pili ya kundi hili lilkuwa na Sajula Lukindo,Onesmo Kibira,Innocent Galinoma,Ben Galinoma, Denis Pad, Francis Kasambala,Vicent na Harry Chopeta, Ally Mwarabu, Sabri Mmanga na wengineo. The Barlocks ni bendi nyingine iliyochipukia Upanga, jina la Barlocks lilitokana na kuweko kwa kundi jingine lililojiita la The Barkeys, kundi ambalo lipo hai mpaka leo ambalo kwa sasa linajulikana kwa jina la The Tanzanites, lililo chini ya Abraham Kapinga. The Barlocks walikuwa wakitumia vyombo vya Barkeys kwani kwa wakati huo bendi hizi zilikuwa kama mkubwa na mdogo. Zamani lilikuwa jambo la kawaida kabisa bendi kuwa na makundi mawili A na B, Dar es Salaam  Jazz Band enzi za Michael Enoch, iliwahi kuwa na Dar es Salaam Jazz Band B, bendi ambayo ilikuwa na mwanamuziki maarufu Patrick Balisdya. Na bendi hii ikawa bora kiasi cha kuwa tishio kwa Dar es Salaam Jazz Band A, ikalazimika Michael Enoch amshauri mwenye bendi kulivunja kundi hilo la pili na kuwaunganisha wanamuziki pamoja, jambo lililomuudhi Patrick na kuwa sababu moja ya kuanzishwa kwa Afro 70. Barlocks hiyo ya awamu ya kwanza ilikuwa na wanamuziki akina Jimmy Jumba, Pimbi Sokoine, huyu alipewa jina la utani Pimbi kutokana na kuwa mrefu sana, Said Mbonde kaka yake Amina Mbonde aliyekuja kuwa muimbaji wa kike mzuri sana pia enzi zake, pia walikuweko Sajula Lukindo na Abraham. Kulikuweko na makundi mengine mengi hapo Upanga, kama vile White Horse, Aquarius ambako ndiko alikotoka producer maarufu Hendrico Figueredo, ambaye pamoja na wenzie walikuja kuanzisha kundi ambalo liko hai mpaka leo linaoitwa InAfrika. Wanamuziki wengine wa Upanga walikuwa akina Joe Ball, Joel De Souza, Mark De Souza, Roy Figueredo, Yustus Pereira, Mike De Souza. Kama unavyoona majina yao hawa walikuwa wengi ni Wagoa, kulikuwa na bendi nyingi za Wagoa katika miaka hiyo kwani hawa walikuwa ni Waasia wa asili ya kisiwa cha Goa, na lugha waliyotumia ilikuwa Kiingereza, hivyo muziki waliokuwa wakipiga ulikuwa wa lugha hiyo.  Baadhi ya wanamuziki niliowataja walienda na kuungana na wanamuziki wengine Arusha na kuvuma sana na kundi lililoitwa Crimson Rage, baadae wakarudi Dar na kujiita The Strange. Leo ukijidai kupiga gitaa Upanga kuna hatari ukaiyiwa polisi kwa kupigia watu kelele.

Comments