KIOO HAKIDANGANYI


PICHA KWA HISANI YA MICHUZI BLOG
Pole muziki wa Tanzania. Pole muziki wa Tanzania uliojitahidi sana kwa miaka mingi kuondokana na dhana kuwa muziki ni uhuni, pole muziki wa Tanzania uliopata kuwa na ushiriki wa nguli kama Marijani Rajabu, moshi William, Muhidin Gurumo, Bi Shakila, Rahma Shally, Jerry Nashon, Raphael Sabuni, David Musa, Patrick Balisdya, na orodha ndefu ya wanamuziki ambao kazi zao zinaheshimika miaka mingi baada ya kutangulia mbele ya haki. Pole muziki wa Tanzania ambao ulikuwa mstari wa mbele wakati wa kupigania uhuru na wanamuziki kama Frank Humplink na dada zake, Salum Abdallah na wenzake, pole muziki wa Tanzania, ambao kwa miaka mingi baada ya Uhuru ulikuwa darasa kwa Watanzania katika kuelimisha kila nyanja ya maisha ya Mtanzania kuanzia siasa, kilimo, ukombozi wa Afrika, na hata afya na chakula bora.  Pole sana muziki wa Tanzania uliokuwa ukitungwa kwa usanifu ili kila mtu mkubwa na mdogo aweze kuburudika na kujifunza mema. Pole ua lililokuwa likitoa harufu nzuri kwa wasikilizaji wote wa Kiswahili, hapa nyumbani na duniani kote. Pamoja na pole zote hizo hakika wanamuziki wa zamani huwezi kutamka kuwa walikuwa malaika wa tabia, la hasha, lakini walilelewa wakijua nini cha kutamka hadharani, hata pale walipoudhiwa sana au walipofurahishwa sana, tungo zao zilifikisha ujumbe bila kutumia lugha isiyoweza kutamkika katika hadhara ya mchanganyiko wa rika. Muziki sasa umejaa wajuzi wa kutunga tungo zilizojaa ukakasi wa maneno na mawazo, unaokufanya ujiulize mtunzi huyu hana wakubwa kwao? Wenyewe hujitetea kuwa uhuru wa kujieleza kwa kusema lililo kichwani kwa lugha yoyote ndio usasa, na kwa kuwa jamii hailalamiki, pengine ndio hali halisi. Mtunzi ni binadamu aliyetoka katika jamii, na hivyo hutunga kutokana na jinsi alivyolelewa na familia yake na jamii iliyomzunguka. Mtunzi aliyelelewa katika mazingira yaliyojaa matusi na lugha sizizo na staha, bila hofu tungo zake zitafuata reli ya malezi yake, na jamii itafurahia kazi hiyo. Wahenga walisema ‘Msanii ni kioo cha jamii’, wengi hukosea tafsiri ya ‘kioo’ hiki na kudhani ni kile ambacho unaona upande wa pili, na hivyo husisitiza kuwa wasanii wabadilike pale wanapoona wasanii hawafanyi yale yanayokubalika katika jamii, bahati mbaya ‘kioo’ kinachozungumziwa kwenye usemi huo ni kile cha kujiangalia sura yako, hivyo basi ukitaka kuijua jamii fulani ilivyo angalia wasanii na sanaa zao. Kama ambavyo ukijiangalia kwenye kioo ukakuta sura mbaya, ujue ndio  sura yako hiyo, kuvunja kioo au kulaani kioo hakutabadilisha sura yako, kazi hapo ni kutafuta wajuzi wa kurekibisha sura, kama ni ndevu wanyoe, kama ni kupaka wanja wafanye hivyo,  kioo hakidanganyi.

Tungo za zamani ambazo zinadumu zilitungwaje? Kwanza kabisa, watunzi walilelewa na jamii iliyokuwa ikijua kuwa kuna maneno ya kutamka hadharani na kuna yale maneno ya faragha, hivyo utunzi wa wasanii hawa  katika bendi au vikundi vya taarab au kwaya ulikuwa wa kufuata maadili ya jamii  yao,  pia vikundi vilikuwa ni chujio zuri la kwanza la kusahihisha pale mtunzi binafsi alipopotoka. Kulikuweko na swala la kupeleka tungo kwenye kamati ya maadili kabla kazi hiyo haijarekodiwa. Kupita chujio hizi kazi zilizotoka zilikuwa na uhakika kuwa hazikuwa na ukakasi  wa kimaadili, japo kwa njia hii ya kamati kulikuwa na mapungufu ya kuzuia kazi kutokana na ujumbe wake badala ya kuhakiki maadili ya tungo. Katika hali ya sasa, mtunzi anakuwa peke yake akitengeneza tungo kadri hisia zake zinavyompeleka, hapo ndipo malezi yake huonekana katika tungo. Tatizo lililopo bila shaka litaendelea kuwa kubwa zaidi kadri siku zinavyoendelea kwani hakuonekani nia yoyote ya kuandaa malezi ya vijana Kitaifa.

Kwa kuwa tuna Waziri mpya wa Utamaduni ni vizuri akaiangalia hali hii na kupanga mikakati ya muda mrefu, kujenga vijana wetu kurudi katika maadili ya Kitanzania. Kati ya mambo ambayo yanggekuwa nyenzo kubwa katika hili ni kuhakikisha elimu ya sanaa inarudishwa mashuleni, sanaa isiwe kitu cha kujifunzia vijiweni na kwenye masikani. Kwa njia hiyo sio tu kwamba tutapata wasanii makini zaidi bali pia tutapata wapenzi wa sanaa makini. Hali hii ya kuachia wafanya biashara kuongoza mwelekeo wa sanaa ni hatari kubwa sana ya kupoteza utu wa Mtanzania. Sanaa ikishakuwa inaendeshwa na biashara, maadili yake hutegemea soko linahitaji nini, na katika ulimwengu wa utandawazi hili ni hatari kwa uhai wa maadili ya jamii ambazo hazina msingi imara wa utamaduni wao. 

Tanzania tunajipanga kuwa Taifa la viwanda, ni muhimu kulea wananchi watakaokuwa wazalendo wa kujivunia vyao au la pamoja na viwanda vyetu tutakuwa soko la bidhaa toka viwanda vya nchi ambazo utamaduni wake utakuwa umejikita katika nchi yetu, sanaa ni njia moja kuu ya kujenga uzalendo, na hivyo pia kujenga wateja wa bidhaa za viwanda tunavyotaka kuvijenga.

Comments