INSPEKTA HARUN ASEMA ANA NDOTO ZA KUJIUNGA NA BENDI KUBWA YA DANSI

INSPEKTA HARUN
UKUMBI wa Sun Diego, Tandika, jijini Dar es Salaam jana ulilipuka furaha ghafla baada ya staa wa Bongofleva, Haroun Kahena ‘Inspekta Haroun Babu’ kuvamia jukwaa la bendi ya JM Mbeta iliyokuwa ikitumbuiza na kuimba nyimbo kadhaa za dansi za zamani.
Kama sinema vile, Inspekta aliyeingia ndani ya ukumbi huo muda mfupi baada ya ratiba ya Mbeta Band kuanza, alikwenda kutulia kwenye meza iliyokuwa pembeni kidogo, kabla ya Kiongozi wa bendi hiyo mwanamuziki mkongwe Julius Mzeru kumkaribisha jukwaani kusalimia.
Akionyesha kujiamini kupita kiasi, Inspekta alipopanda jukwaani alikamata kipaza sauti akatoa salamu kwa mashabiki pamoja na kuwashukuru Mbeta Band kwa kumpa heshima hiyo, kisha akaomba apigiwe kibao chochote alichoimba Bichuka.
Kama waliopanga vile, mara moja wanamuziki wa Mbeta wakaanzisha ala ya wimbo ‘Siwazuri Binadamu’ wa bendi ya OSS na kujikuta wamewainua watu na kuwavuta kati kucheza, huku wengine wakipigana vikumbo kumtuza Inspekta aliyekuwa akiimba kwa hisia kali.
Baada ya wimbo huo, ili kuwaridhisha mashabiki walioonekana kuwa bado wana kiu ya kumshuhudia Inspekta akiimba muziki wa Dansi, Mbeta Band wakaanzisha ala ya kibao ‘Sauda’ cha DDC Mlimani Park ‘Sikinde’. Blog hii iliongea na Inspekta baada ya kushuka jukwaani, ambapo alisema kuwa, ni kawaida yake mara kwa mara kutembelea bendi za Dansi na kupanda jukwaani kusalimia kwa staili ya uimbaji.
“Nimeshafanya hivyo kwa karibu bendi zote hapa nchini, zikiwamo zile kubwa kama vile; FM Academia, Twanga Pepeta, Malaika Band Msondo Ngoma na Mlimani Park Sikinde,” alisema Inspekta.
Alisema kuwa, kitendo chake cha kupanda kwenye majukwaa ya bendi za Dansi ni hatua za awali za ndoto aliyonayo ya kujiunga na moja ya bendi kongwe za miondoko hiyo hapa nchini.

Comments