HARAKATI ZA WASANII KUPATA NAFASI KATIKA KATIBA MPYA—1


MHE. PAULYNUS RAYMOND MTENDA
Kuna mashirikisho manne ya sanaa nchini ambayo ni Shirikisho la muziki, Shirikisho la Filamu, Shirikisho la Sanaa za maonyesho na Shirikisho la Sanaa za Ufundi. Ulipotolewa wito wa makundi maalumu kutoa mapendekezo yao katika Katiba Mpya,  Mashirikisho yalikaa kama Kamati za katiba na kuja na mapendekezo kadhaa kwenye katiba, mapendekezo hayo licha ya kupokelewa na Tume ya Katiba hakuna kilichoingizwa katika Rasimu ya Katiba.
Baada ya hapa ndipo wito ukatolewa wa kupendekeza majina ya watu watakaoingia katika Bunge la Katiba, Mashirikisho yote yalipendekeza majina mbalimbali. Hatimae jina la Paulynus Raymond Mtenda lilirudi kama ndie mwakilishi aliyeweza kutoka katika kundi la Watu wenye malengo yanayofanana .
Tarehe 14, February 2014 viongozi wa Mashirikisho walikutana BASATA kumpongeza Mbunge Mteule huyu na kumkabidhi rasmi mapendekezo ambayo yalipelekwa awali kwenye Tume ya Katiba ili aweze kuyapendekeza katika katiba mpya.

NAIBU KATIBU MTENDAJI WA BASATA AKIMKABIDHI MBUNGE MTEULIWA MAPENDEKEZO YA MASHIRIKISHO
Pamoja na mapendekezo hayo Shirikisho la Filamu TAFF, na Mtandao wa Wanamuziki Tanzania (TAMUNET), pia walikuja na hoja mbili muhimu nazo ni;
1.     Kutambuliwa kwa wasanii kama ni kundi maalumu katika Katiba, kama yalivyoweza kutambuliwa makundi ya wakulima, wavuvi na wafanyakazi. Sababu kubwa za kuja na hoja hii ni kutokana na ukweli unaopatikana katika tafiti mbalimbali.  Wasanii ni wengi sana, katika ripoti ya BASATA ya mwaka 2006, idadi ya wasanii nchini wakati huo ilikuwa kiasi cha milioni sita. Kwa kuwa ni maka minane sasa imepita toka wakati wa ripoti hiyo kuna kila sababu ya kuamini kuwa kundi hilo limekuwa kubwa zaidi. Sababu nyingine ni ukweli kuwa wasanii wanasababisha ajira kwa kundi kubwa la watu, wakiwemo wafanyakazi wa vyombo vya utangazaji, wafanya kazi katika biashara ya matangazo, wasambazaji, wafanya biashara ndogondogo, (machinga) na wengine wengi waliomo katika mnyororo wa biashara hii ikiwemo, maproducer, mameneja, mafundi mitambo, watayarishaji wa maonyesho na kadhalika. Hivyo sanaa si utamaduni tu bali ni kazi yenye mapato makubwa. Ripoti ya WIPO ya mwaka 2012 imeonyesha kuwa kazi zitokanazo na Hakimiliki huingiza fedha nyingi zaidi katika uchumi wa Taifa kuliko MADINI, jambo ambalo ni wazi wengi wanaosikia kwa mara ya kwanza hushangaa kwa kuwa kelele za mapato ya Madini ni kubwa sana katika jamii wakati hakuna anaelalamika kuhusu mapato kutokana nah ii raslimali ya nchi inayoitwa sanaa. Ripoti hiyo ya WIPO pia ilionyesha kuwa sekta ya Hakimiliki inaajiri watu wengi zaidi kuliko, sekta za Madini, gesi, maji, Ustawi wa Jamii, Afya, Usafirishaji. Hivyo ni sekta ambayo ina umuhimu sana katika uchumi wa Taifa  ikiwa italindwa inavyostahili.
2.     Hoja ya pili ilikuwa kuwekwa rasmi kipengele cha kutambuliwa kwa MIliki Bunifu na kuhakikishiwa ulinzi na uendelezaji wa shughuli za Milikibunifu katika Katiba. Wasanii hutegemea maendeleo yao na uboreshaji wa kazi zao kwa kulindwa kwa Hakimiliki. Lakini ingekuwa ni uchongo wa mawazo kudai ulinzi wa Hakimiliki peke yake. Hivyo lengo ni kupata ulinzi wa Miliki bunifu ambayo itasababisha kulinda haki za wasanii ,wabunifu, wagunduzi, wanasayansi na teknolojia mbalimbali. Kuna mifano kila mara hutolewa ambayo inaonyesha nchi kadhaa ambazo wakati nchi hii inapata Uhuru, uchumi wan chi hizo nasi ulikuwa sawa, kama vile Malasia, Thailand na korea Kusini ambazo kutokana na ulinzi  na uendelezaji wenye mipango wa Miliki Bunifu nchi hizo zimewezesha uchumi wao kukua na kuwa katika chumi bora duniani

Comments