Ijue kazi ya meneja wa mwanamuziki


Talent Manager au pia anayejulikana kama Artists Manager au Band Manager, ni mtu au kampuni mwenye kazi ya kumuongoza msanii katika taaluma yake. Pia kazi yake ni kufuatilia biashara za msanii kila siku na kutoa ushauri na muongozo kuhusu mipango ya muda mfupi na mrefu ya msanii na hata maamuzi ya kibinafsi ambayo yanaweza kuathiri kazi ya msanii, kama vile tabia za matusi, ulevi, uchelewaji kazini nakadhalika. Meneja humsaidia msanii kupata Talent Agent na hata kushauri kuachana na agent aliyepo, Meneja pia kazi yake kubwa ni kutoa ushauri kuhusu maonyesho, promotion, mikataba mingine ya kibiashara, mikataba ya kurekodi na kadhalika.. Agents ndio wanaoingia mikataba kwa niaba ya wasanii, meneja huwa mshauri tu wa mikataba hiyo.
Meneja mara nyingi huajiriwa na Bendi au mwanamuziki, au mara nyingine meneja hugundua kipaji cha mwanamuziki na wakaanza mahusiano ya msanii na meneja, mahusiano haya kwa kawaida huhalalishwa kwa mkataba wa maandishi ambao hueleza wazi mipaka na majukumu ya meneja na mwanamuziki kwa upande wake. Kwa kawaida meneja hulipwa kwa kamisheni, hii kwa kawaida huwa kuanzia  15% ya mapato ya msanii yaliyotokana na juhudi za meneja, kwa meneja mzuri kazi zote za msanii huwa zimepitia mikononi mwake. Nimeona leo niongelee kuhusu mameneja bada ya hasa kusikia vituko vya mameneja wa wanamuziki fulani maarufu wiki chache zilizopita, ambao waliwakosesha wanamuziki wao nafasi ya kushiriki jukwaa moja na wanamuziki wa jazz wenye heshima kubwa katika muziki wa jazz duniani, kwa kudai vitu ambavyo haviwezekani.
Maquis Original
Bendi nyingi zilianza kwa kuwa na aliyejulikana kama Katibu wa bendi, huyu kimsingi alikuwa akifanya kazi nyingi za meneja wa bendi, ila alikuwa mmoja wa wanamuziki, ambaye pia alifanya shughuli ya Ukatibu wakati wa mikutano ya bendi, hakuwa na mkataba tofauti na wanamuziki wenzie ila mara nyingi alikuja kuwa na nguvu sana kwa kuwa yeye ndie aliyekuwa na maamuzi mengi ya matumizi ya pesa za bendi.
 Karibuni kumekuweko na taratibu za bendi kuwa na  mameneja ambao wengi hulipwa mshahara, lakini kazi zao haziko sawa na mameneja wengine wa muziki duniani, maana mara nyingine ni vigumu kutambua nani mkubwa kati ya meneja na mwanamuziki, ambaye kimsingi ndie muajiri wa meneja.
Wiki chache zilizopita kulikuweko na Tamasha la muziki wa Jazz, wanamuziki wenye uzoefu mkubwa walikuwepo hapa nchini, japo ni wazi promo ya Tamasha hilo aidha haikuwa nzuri, au ililengwa kwa kundi fulani la Watanzania tu kwa hiyo wengi hawakulijua, hata wanamuziki wengi wapenzi wa Jazz na wapigaji wa muziki wa jazz, hawakuwa na taarifa kuhusu tamasha la Jazz ambalo lilikuwa likiendelea jijini Dar es Salaam. Hata hivyo nilipenda kuwaasa wanamuziki kuwapa semina mameneja wao kuwa katika maendeleo ya muziki si kila mara lazima udai malipo. Leo hii mwanamuziki kuambiwa ufanye onyesho na mwanamuziki ambaye amekwishafanya kazi na wanamuziki walio katika ngazi za juu za muziki duniani ni muhimu, inasaidia kupata uzoefu na kujifunza mengi mapya, na pia  huwezi kujua matokeo ya kukutana huko. Mameneja kadhaa walikataza wanamuziki wao kupanda jukwaani na wanamuziki waliokuwa nchini kutoka Marekani na Afrika ya Kusini, sina uhakika kama wanamuziki wenyewe wangekubaliana na uamuzi huo wa mamenjea wao. Meneja anatakiwa aangalie faida za onyesho kwa muda mrefu na si kujali laki mbili ya mara moja ambayo inamdhalilisah mwanamuziki.


Comments