JAY Z ALIPOAMUA KUUCHANA KI HIP HOP UONGO WA KIHISTORIA




Na Moses Gasana
Mwezi wa nne mwaka huu wanamuziki Jay Z na Beyonce, ambao ni mume na mke wakibarikiwa kuwa na mtoto mmoja, walifanya safari ya kwenda Cuba kwa mapumziko katika kusherehekea miaka mitano ya ndoa yao. Safari hiyo iliibua mjadala mkubwa miongoni mwa raia wa Marekani na watu wengine wa Ulaya, Amerika ya Kusini, Asia na Afrika.



Kilicholeta mjadala miongoni mwa Wamarekani wenyewe kuhusu safari ya Jay Z na Beyonce ni kutokana na ukweli kuwa kuna masharti magumu ya kisheria ili mtu aweze kuruhusiwa kwenda nchini Cuba. Hii ni kutokana na kuwa kwa miaka 51 kisiwa cha Cuba kimekuwa chini ya vikwazo vya kiuchumi kutoka kwa serikali ya Marekani. Mojawapo ya vikwazo hivyo ni kwamba raia wa Marekani haruhusiwi kusafiri kwenda Cuba kama safari yake hiyo haihusiani na masuala ya elimu, utamaduni au misaada ya kibinadamu. Sasa kwa safari ya Jay Z na Beyonce swali ikawa ‘imekuwaje hawa wapenzi tunaona wako Cuba kama watalii, wakati safari ya utalii hairuhusiwi?’. Hapa lazima uzingatie kuwa utalii unaingiza fedha za kigeni katika nchi, na serikali ya Marekani ilishaweka vikwazo vya kuhakikisha Cuba haipati fedha za kimarekani zinazoweza kupatikana kwa njia za biashara ikiwemo utalii. Maswali yakazidi, ‘hawa wapenzi wamewezaje kwenda kutembea Cuba? nani kawaruhusu?’
Japo ilikuja kujulikana kuwa Jay Z na Beyonce walipata kibali kutoka serikalini cha kwenda Cuba kwa kigezo cha safari ya kitamaduni zaidi, lakini muonekano wao kule ukaacha taswira ya wapenzi waliokwenda kama watalii. Hii ilisababisha hata wanasiasa fulani kutoa maoni ya kutaka ati wapenzi wale washtakiwe kwa kuvunja sheria. Kwa wengine wengi, safari ya Jay Z na Beyonce imeongeza chachu kwenye  mjadala wa kutaka vikwazo vya kiuchumi dhidi ya Cuba viondolewe kabisa.
Hata Jay Z mwenyewe katika kuwajibu waliopinga safari yake ile akatoa wimbo mmoja unaoitwa Open Letter (Barua ya wazi) kuwajibu vikali na kushutumu sera ya Marekani dhidi ya Cuba. Katika mstari mmoja anasema,
“…I’m in Cuba, I love Cubans
This communist talk is so confusing
When it’s from China, the very mic that I’m using…”
Kwa wanaojua historia ya sera ya Marekani dhidi ya Cuba, mashairi ya Jay Z ni ngumi nzito dhidi ya uso wa udhalimu. Inakuwaje Marekani isitake kufanya biashara na Cuba kisa eti ni nchi ya kikomunisti na inakandamiza haki za binadamu lakini ikawa tayari kufanya biashara na China au Vietnam ambazo ni za kikomunisti. China kila kukicha inashutumiwa na Marekani kwa kuvunja haki za binadamu lakini biashara baina yao zinaendelea usiku na mchana!!
Kihistoria, Marekani iliiwekea Cuba vikwazo mwaka 1960 wakati huo rais akiwa Dwight D.Eisenhower. Hasira hii ilitokana na kutaifishwa kwa makampuni ya kimarekani takribani 5,911 yaliyokuwa yakifanya shughuli za kiuchumi nchini Cuba. Hiyo ilitokana na uamuzi wa Fidel Castro baada ya kuchukua nchi, kufuata siasa za kikomunisti na kuweka misingi mikuu ya uzalishaji mali na uchumi chini ya usimamizi wa serikali. Biashara huria ya kibepari ikawa imepigwa konde la nguvu.
Makampuni ya kimarekani yaliyokuwa yakifanya biashara ndani ya Cuba yalilaumiwa kwa kuvuna faida kubwa na kuiachia Cuba kilicho kidogo.Hata Kennedy wakati akiwa mgombea urais alilaumu sera ya Rais Eisenhower juu ya Cuba kwa kutumia nguvu na ushawishi wa serikali kuyasaidia makampuni yale kuikamua Cuba badala ya kuhakikisha nayo inastawi kiuchumi. Pia Kennedy alilaumu sana serikali ya Marekani kuusaidia utawala dhalimu wa dikteta Batista. Sio ajabu basi Castro hadi leo kwa kiasi kikubwa anamheshimu marehemu Kennedy kama rais aliyekuwa anajua vyema hali halisi ya maisha ya wacuba, japo naye ilimbidi tu afuate hivyo hivyo kwa shingo upande sera ya Marekani kwa Cuba.
Marekani ilichukia na kuamua kufunga milango ya ushirikiano na Cuba. Hakuna mmarekani anaruhusiwa kufanya biashara na serikali ya Cuba. Lengo la vikwazo hivi ikiwemo kutoruhusiwa kusafiri kwenda Cuba ni ili kudhoofisha uchumi wa Cuba ili wananchi wake waung’oe utawala wa Fidel Castro (Hivi sasa Castro ni mstaafu). Hata hivyo kwa umahiri mkubwa serikali ya kimapinduzi ya Cuba ikatokea kuwa mfano wa kuigwa dunia nzima katika ujenzi wa nchi hasa huduma za jamii.Watu wengi duniani wanajua namna Cuba ilivyojenga uwezo katika masuala ya huduma za afya na matibabu, elimu, miundombinu na hata uwezo wa kijeshi.
Kwa miaka mingi Cuba imekuwa ikitoa madaktari na walimu wake bure kwenda kusaidia nchi mbalimbali ili kujenga mifumo ya utoaji huduma za afya, matibabu na elimu. Madaktari hao hao huenda hata huko Marekani ili kusaidia utoaji wa matibabu kwa wananchi. Kijeshi Cuba ilizisaidia sana Angola, Msumbiji na Namibia miaka ya 1970 kutembeza kichapo dhidi ya makaburu wa Afrika ya Kusini. Hadi leo kichapo walichotoa wacuba dhidi ya majeshi ya Afrika Kusini mwaka 1975 nchini Angola hakitasahulika kamwe (soma kuhusu Operation Carlota). Tanzania tunamkumbuka mcuba Brigadier Walden (marehemu sasa) aliyeshiriki katika kuongoza vita ya kumng’oa Idi Amin mwaka 1978-79.
Kisiwa cha Cuba kina ukubwa wa kilometa za mraba 100,000 na idadi ya watu inayokadiriwa kuwa kama milioni 11.
Mambo mengi sana yameshatokea katika huu mvutano mkongwe kati ya Cuba na Marekani. Mwaka 1962 almanusura vita ya tatu ya dunia ilipuke baada ya Urusi kuweka makombora ya nyuklia kisiwani Cuba..Katika mgogoro huo wa makombora (The Cuban Missile Crisis) Marekani ilipinga vikali ukitilia maanani kuwa Cuba iko umbali wa kilometa 150 tu kati yake na Marekani (Kama maili 93). Urusi ilifanya vile ili kukilinda kisiwa cha Cuba dhidi ya uvamizi mwingine kutoka Marekani.Hapa ikumbukwe kwamba mwaka mmoja nyuma, mwaka 1961, kulifanyika uvamizi uliosaidiwa sana na Marekani wa kutaka kuiondoa madarakani serikali ya Fidel Castro (Playa Giron Invasion).Uvamizi ule ulikwama baada ya kupokea kipigo kutoka kwa majeshi ya Cuba huku Castro mwenyewe akishiriki kikamilifu katika uwanja wa mapambano kwa kuelekeza hiki na kile hadi ushindi. Hivyo mwaka 1962 Urusi ikakubali kuziondoa meli zilizokuwa zimebeba makombora yale ya nyuklia kutoka Cuba na ikawa mwisho wa hofu ya kuzuka vita kubwa.
Lakini ukweli ni kwamba Cuba iliendelea kuishi huku ikikabiliwa na uchokozi mwingi sana kutoka Marekani. Wacuba waliokuwa wanampinga Castro ambao wanaishi Florida nchini Marekani wameendelea kusaidiwa kwa fedha na  rasilimali zingine ili kuidhoofisha serikali ya kimapinduzi ya Cuba. Katika mojawapo ya uchokozi huo ni majaribio lukuki ya kumuua Fidel Castro. Katika kitabu chake kiitwacho “My Life” Fidel Castro anaulizwa na mwandishi Ignacio Ramonet kama anajua idadi kamili ya majaribio ya kumuua. Castro anamjibu kuwa labda siku akienda mbinguni kuonana na Mungu ndipo ataweza kujua idadi kamili ya majaribio hayo. Hata hivyo Ignacio Ramonet anaweka idadi ya majaribio kuwa ni 600. Kuanzia kutegeshewa sumu hadi milipuko. Tazama vile vile filamu (documentary) iitwayo 638 Ways to Kill Castro yenye kueleza mikakati michafu ya shirika la kijasusi la Marekani CIA dhidi ya Castro.
Njia zingine ambazo zimekuwa zikitumiwa na Marekani ili kuidhoofisha serikali ya Cuba ni kuruhusu wacuba ambao wanatumia njia zisizo halali kuingia Marekani kupata upendeleo fulani na kuruhusiwa kubaki huko. Huu mkakati umewekwa hadi katika sheria (Cuba Adjustment Act) kiujanja ili uweze kuhamasisha wimbi la wacuba kuikimbia nchi yao ili kuweza kutengeneza mazingira ya serikali kuondolewa. Mkakati huu mchafu nao kama mingine umefeli kwa miaka mingi.
Mbinyo wa serikali ya Marekani dhidi ya Cuba umekuwa ukiendelea kwa miaka 51 hadi sasa.  Vikwazo hivi vya kiuchumi vimekuwa vikilaaniwa sana na Umoja wa Mataifa kwa miaka mingi mfululizo huku Marekani ikiziba masikio.Kwa mfano, mwaka 2006, katika kura 183 kwa 4, Umoja wa Mataifa uliitaka Marekani kuondoa vikwazo vya kiuchumi na biashara vilivyowekwa dhidi ya Cuba. Marekani hadi sasa haijafanya hivyo japo rais Obama anatajwa kulegeza kidogo mbinyo huo.
Katika marais waliopita wa Marekani Bush alitia fora zaidi kwa ubaya dhidi ya Cuba. Kama kawaida yake alidiriki hata mwaka 2004 kuiweka Cuba katika orodha ya nchi zinazounga mkono ugaidi na kudai kuwa ina mpango wa kutengeneza silaha za sumu za kibaiolojia. Tukumbuke kuwa ni Bush huyu huyu aliyedai Iraq ina silaha za maangamizi ya halaiki lakini hadi leo hakuna ushahidi wowote uliounga mkono madai hayo.Sana sana alifanikisha lengo lake la kumuua Saddam Hussein. Lakini Bush bila shaka ni mnafiki namba moja duniani kwani Marekani imefadhili ugaidi dhidi ya Cuba kwa kiwango kikubwa ukiacha mbali ugaidi dhidi ya mataifa mengine ya Marekani ya Kusini kama Guatemala na Nicaragua. Kwa taarifa zilizopo mitandaoni ugaidi huo dhidi ya Cuba umeua zaidi ya watu 3,500 nchini Cuba na kuacha watu takribani 2,000 wakiwa na ulemavu. Bush analijua hilo wazi. Huyo ndiye Bush na hiyo ndiyo Marekani “mtetezi wa haki za binadamu namba moja”.
Jay Z bila shaka kwa kusukumwa na mapenzi yake makubwa kwa falsafa za Che Guevara ameamua kuukataa uongo mkubwa wa kihistoria wa sera ya Marekani dhidi ya Cuba. Labda kwa ufupi tu, Che Guevara alijipatia sana sifa na kupendwa dunia nzima pale kwa kushirikiana na Fidel Castro na wananchi wengine wa Cuba walipofanikisha vita ya msituni na kumwondoa dikteta Batista mwaka 1959 na kuunda serikali ya kikomunisti nchini Cuba.Baada ya hapo Che Guevara alipita nchi mbalimbali akisaidia harakati za kimapinduzi za wanyonge hadi alipokamatwa katika mapambano nchini Bolivia na kuuawa mwaka 1967.
Jay Z kwa wimbo wake wa Open Letter ameamua kuwapiga kwenzi wapotoshaji wa historia. Anasema,
“…Politicians never did shit for me
Except lie to me, distort history…”
Hakika wamarekani kwa miaka mingi wamelishwa historia ya uongo kuhusu mgogoro wa nchi yao na Cuba. Propaganda chafu za kudhoofisha maendeleo ya kisiwa cha Cuba zimedumu kwa miaka mingi na sasa zimeanza kuwaudhi vijana kama Jay Z. Hivyo bila shaka kwa ukali wa mashairi na ngoma nzito za Hip Hop mjadala wa kutaka Cuba iondolewe vikwazo umepata nguvu na ari mpya. Hongera Jay Z na Beyonce kwa safari yenu Cuba na Mungu awajalie safari nyingi tu za kuadhimisha miaka mingine ya ndoa yenu.
Na Moses Gasana
Mawazo Chanya Media
0713480670

Comments

Unknown said…
Makala nzuri sana. Hongera