MAAJABU YA KABURI LA KANUMBA NA GOBBY


Nilipatwa na mshangao mkubwa baada ya kukumbuka jambo lililosahaulika na pengine kutofahamika kwa wengi la marehemu Isiaka Gobby linalofanana sana na tukio la Steven Kanumba
Hatua chache baada ukiingia katika lango la makaburi ya Kinondoni, kushoto kwako utalikuta kaburi la msanii Steven Kanumba. Kanumba akiwa na umri mdogo wa miaka 28, alifariki ghafla katika mazingira ambayo yamepelekea msanii mwenzie  Elizabeth Michael kuwa katika kesi ya kutuhumiwa mauaji ya msanii huyu aliyekuwa mahiri katika kazi yake ya usanii wa kuigiza na pia aliyekuwa na sura ya kupendeza yenye mvuto, wengi tunamfahamu kwani bado yuko katika mawazo yetu kutokana na kazi zake kuwa bado zikiendelea kuonekana katika vyombo mbalimbali vya utangazaji. Jirani kabisa ya kaburi la Kanumba, kuna kaburi moja la zamani sana la mwanamuziki Isihaka Gobyy.  huyu alikuwa mwanamuziki wa Orchestra Makassy katika miaka ya 1976/77. Gobby nae alikuwa na sifa zilizofanana sana na zile za Kanumba. Kwanza alikuwa mwanamuziki muimbaji mahiri sana, pili alikuwa na sura yenye kuvutia sana.
 Wakati huo bendi ya Makassy ikiwa na makao makuu ukumbi wa Hunters, ikiwa na ushindani mkubwa kutoka kwa bendi ya Bana Ngenge iliyokuwa  katika ukumbi mwingine jirani wa Savannah, na Orchestra Maquis du Zaire iliyokuwa ikipiga katika ukumbi wa Resort Kimara.
Gobby nae alikufa kifo cha ghafla akiwa na miaka 28, kwa kuuwawa kwa kupigwa na hatimae kuchinjwa kama kuku katika ugomvi uliovuma wakati huo kuwa ulikuwa ukihusu mapenzi. Hakuna taarifa za kuwahi kukamatwa aliyemfanyia Gobby unyama huu uliopoteza maisha yake mwanamuziki huyu kijana.
Mungu awalaze Kanumba na Gobby Pema Peponi

Comments