UMUHIMU WA UTUNZAJI WA VYOMBO VYA MUZIKI


Jana niliingia katika duka moja la vyombo vya muziki na nikawa na maongezi marefu na mwenye duka, kati ya mambo ambayo tulizungumzia ni tatizo la watu kuamua kufanya  shughuli za muziki na kuanza kununua vyombo bila kutaka ushauri wa wataalamu wa mambo ya  vyombo vya muziki. Nimeona leo nizungumzie hilo. Kwanza kabisa kumekuwa na tatizo kubwa la kuweko kwa vyombo ‘feki’ katika maduka kadhaa ya vyombo vya muziki. Hivyo si kila chombo kikiwa na nembo ya Yamaha ni kweli chombo kutoka kampuni hiyo, kwa kweli asilimia kubwa sana ya vyombo vya muziki ni feki. Ili kugundua  hilo ni muhimu kutumia wataalamu wa vyombo vya muziki. Mfano wa karibu ni mdau mmoja anaeendesha bendi, kujikuta amekwisha nunua vyombo mara 3 katika miaka mitatu kutokana na vyombo anavyounua kutokukidhi viwango vinavyotakiwa. Kwa taarifa zilizopo ni kuwa mara ya kwanza aliuziwa na tapeli aliyejidai katoka Uingereza na vyombo original toka huko, kwa kuwa hakutumia wataalamu alijikuta vyombo alivyovinunua havina sauti yenye ubora, na si muda mrefu alikuja gundua kuwa kila kitu alichouziwa kilitengenezwa na mafundi seremala toka Mwananyamala.
Ni vizuri kabla ya kutumia mamilioni ya fedha kununua vyombo kutafuta wataalamu ambao wapo kadhaa hapa nchini ukawaeleza matakwa yako nao wakakupa ushauri wa kitu gani ununue na baada ya hapo hata kushiriki kuvifunga na kutoa semina fupi ya utunzaji wa vyombo hivyo kwa mafundi wa bendi na pia wanamuziki wa bendi.
Si kila mwanamuziki ni mtaalamu wa vyombo bora, si mara moja utasikia mfanya biashara kasindikizana na mwanamuziki kwenda kununua  vyombo na baada ya muda mfupi vyombo hivyo huharibika. Tatizo jingine la ajabu kabisa katika utunzaji wa hivi vyombo, mtu akinunua gari la shilingi milioni tatu, kamwe hawezi kumkabidhi mtu yoyote barabarani aliendeshe gari lake. Lakini utaweza kukuta mtu ananunua vyombo vya muziki vya shilingi milioni kumi na tano na haoni tabu kumuita ndugu yake na kumwambia awe ndie fundi mkuu, kwa vile tu ndie huwa anabadilisha balbu nyumbani kwake. Na si ajabu hata kidogo kukuta mafundi mitambo katika bendi nyingi ndio wanaopata mshahara mdogo kuliko msanii mshiriki mwingine yoyote katika bendi. Hii imetokana na kuwa mafundi mitambo wengi walianza kazi katika bendi kama wabeba vyombo, baada ya kujua waya gani unaingia wapi, hupanda cheo na kuwa mafundi mitambo. Matokeo ni muziki wenye sauti mbovu na vyombo kufa mapema hata kama ni bora.
Kampuni mbalimbali huwa na utalaamu unaozidiana katika kutengeneza vyombo. Kuna kampuni ambazo ni mahiri katika kutengeneza vifaa vya studio, lakini vifaa vya kampuni hiyohiyo ukitaka kuvitumia maonyesho ‘live’ aidha vitakuwa havina ubora wa sauti au vifaa hivyo kuharibika mapema.  Kuna majina ya kampuni ambazo ni mahiri katika vifaa  vya aina fulani kwa mfando Roland ni mahiri sana kwa vinanda, ni vizuri kujaribu kupata vinanda vya kampuni hiyo kwani huwa vinavumilia sana mikiki mikiki ya bendi zetu. Kwa bendi ambazo zinahitaji kupata amplifaya kwa ajili ya magitaa, ni ushauri mzuri kutumia combo aina ya Marshal au Fender, japo kweli vifaa hivi ni gharama sana lakini kampuni hizi zina historia ya umaarufu wa kutengeza amplifaya kwa ajili ya wapiga magitaa wa muziki wa rock, ni aina ya mashine ambazo zinaweza kutoa sauti inayofaa kwa ajili bendi zetu. Kwa upande wa gitaa la bezi ningeshauri mashine za Lanney kampuni hii hutengeneza mashine bora za bezi. Kuna kampuni ambazo ni maarufu kwa utengezaji wa mixer bora kwa ajili ya maonyesho live. Soundcrafters na Yamaha ni kati ya kampuni zenye mixer bora. Magitaa hutengezwa na kampuni nyingi sana, lakini kuna kampuni kama Fender na Ibanez ambazo huteneza magitaa mazuri yenye pickup zenye nguvu na ambazo zinadumu.
Pamoja na ushauri huu ni muhimu kupata mtaalamu kwani kila kundi huwa na mahitaji tofauti, yanayo husu aina ya muziki, ukubwa wa sehemu ambayo maonyesho yanategemewa kufanywa na kadhalika.  Vyombo vya muziki ni gharama sana na ndio jembe la bendi, vikitunzwa vizuri vinaweza vikatumika kwa miaka mingi bila matatizo, ni muhimu kufuata masharti yanayotolewa na fundi mwenye uelewa

Comments

Unknown said…
Sawa sawa, nina swali nalo ni juu ya ultimate ear or ear mornitor, zinapatikana tanzania? Na kwa gharama gan?