WATANZANIA WATATU KUSHIRIKI KORA MUSIC AWARDS


Kora All Africa Music Awards 2012 hatimae zimefika. Nimeona niandike kidogo kuhusu hili kwani safari hii wasanii watatu toka Tanzania wameteuliwa kushiriki katika kinyang'anyiro cha tuzo hizo nao ni Saida Karoli, Ally Kiba, na Dogo Aslay ambaye kwa sababu ambazo sijazijua ametajwa kama mshiriki kutoka Kenya. Tuzo za mwaka huu ziko katika makundi 21, wasanii wa Tanzania watashindana katika makundi matatu kama ilivyo hapo chini;

1.     Best Male Newcomer of the African continent- ambapo Dogo Aslay na wimbo wake Niwe nawe, atapambana na wasanii wengine watano, Floby  wa Burkina Faso, Aziz Azion wa Uganda, John Chiti wa Zambia, Loyiso wa Afrika ya Kusini na Davido wa Nigeria.
2.     Best Male Artist of East Africa- katika kundi hili ndipo Ally Kiba anagombea tuzo huo kwa wimbo wake Single Boy ambao alimshirikisha Lady Jay Dee, wengine waliomo katika kinyang’anyiro hicho ni Jimmie Gait wa Kenya,Chris D wa Burundi, Kidum wa Burundi, Redsan wa Kenya na Mulatu Astatke wa Ethiopia
3.     Best Female Artist of East Africa- ndilo kundi tunalomkuta Saida Karoli akigombea kinyang’anyiro hicho na wimbo wake  wa Sakina, washindani wengine ni Juliana Kanyomozi wa Uganda, Helen Berhe wa Ethiopia, Marya wa Kenya, Asther Aweke wa Ethiopia na Ikraan Caraale wa Somalia
Dogo Aslay

Ally Kiba

Saida Karoli
Tuzo za Kora  zilianza kwa mara ya kwanza 1994, zikiwa wazo la mfanya biashara Ernest Coovi Adjovi, mzaliwa wa Benin. Kwa mara ya kwanza Tuzo sherehe za tuzo hizi zilianza kufanyika nchini Afrika ya Kusini, na kwa miaka ya kwanza zilikuwa na mgogoro kutokana na kuwa na washindi wa kwanza wote kutoka nchi zinazozungumza Kifaransa tu, na kwa mara ya kwanza mshindi alipotoka nchi zinazozungumza Kiingereza wale wanamuziki kutoka nchi zinazozungumza Kifaransa wakatishia kutoshiriki Tuzo hizo. Pamoja na migogoro yote hiyo ya kukua, KORA Awards zimekuwa kama Grammy Awards kwa nchi za Afrika na Diaspora yake.
Mwaka huu kaulimbiu ya Tuzo hizi ni Amani Afrika, na shughuli nzima itafanyika katika hoteli moja kubwa sana iliyoko Abidjan Ivory Coast. Palais des Congres de l’Hotel Ivore siku ya Desember 2012.

Comments