Wapi gitaa la rythm siku hizi?


Marehemu Kassim Karuona wa Tabora Jazz, mmoja wa wapiga rythm aliyekuwa bora Tanzania.
Katika mfumo wa awali bendi za Tanzania, zilikuwa zikitumia si chini ya magitaa matatu, Solo, rythm na Bass, nasema matatu kwa kuwa kulikuwa na bendi ziliwahi kufanya majaribio ya kuwa na mgitaa zaidi kama ntakavoeleza hapo chini. Gitaa la solo lilikuwa na sauti ya juu, huku rythm ikiwa na sauti nzito kidogo ya kati, na mwisho Bass likiwa na sauti nzito kuliko magitaa mengine. Kimuundo gitaa la rythm na la solo hakuna tofauti. Yote yana nyuzi 6,lakini katika kutyuni kwenye amplifier, gitaa la rythm hunyimwa treble kiasi na kuongeza bass zaidi kuliko gitaa la solo ambalo huwa na treble zaidi ya magitaa mengine. Inasemekana kaka yake Dr Nico, ndie aliyeanzisha mtindo wa kuongeza gitaa la nne lililoitwa second solo. Hili lilikuwa likipigwa kwa mifumo mbalimbali katika bendi mbali mbali. Bendi nyingine zilitumia second solo kama gitaa lililokuwa linajibizana na solo, na bendi nyingine lilikuwa linajibizana na rythm. Bendi ya Cuban Marimba chini ya Juma Kilaza liliongeza ubunifu na kuongeza gitaa la 5 na kuliita chord guitar, kadri unavyoongeza magitaa unahitaji ubunifu zaidi katika utunzi ili kuweza kutoa nafasi magitaa yote yasikike na pia kila gitaa lipige kitu chake lakini kiwe na uhusiano na magitaa mengine. TP OK Jazz ilibadili mchezo kukawa na solo mbili, Mzee Franco akipiga solo na pia wapigaji kama Mavatiku nao wakipiga solo katika wimbo huohuo lakini wakigawana vipande vya kupiga.
Lakini leo tuzungumzie gitaa la rythm. Chombo hiki bado kinapigwa katika bendi nyingi lakini umaaarufu wake umeshuka sana. Naona wapigaji wake hawapewi umuhimu, na unaweza kuingia katika asilimia 90 ya bendi ukamuona mpiga rythm lakini husiki anapiga nini kutokana na kelele zinazoruhusiwa kuendelea katikati ya muziki. Katika kipindi cha miaka ya 60 na 70, gitaa hili lilikuwa na umuhimu mkubwa na wapigaji wake waliweza kubuni staili zao wenyewe. Kati ya wapiga rythm maarufu namkumbuka Satchmo, hilo ndio lilikuwa jina la kisanii la Harrison Siwale mpiga rythm wa Jamhuri Jazz, yeye alikuwa na staili peke yake ya kupiga rythm, sikumbuki kusikia mtu mwingine akipiga rythm ya aina yake kabla ya hapo. Rythm yake ilitawala nyimbo za Jamhuri wakati huo. Kumbuka wimbo kama Mganga no 1 na 2, au Blandina. Marehemu Mzee Kasim Kaluwona nae alikuwa na staili tofauti ya upigaji uliyoifanya Tabora Jazz kuwa na staili yake peke yake, kumbuka gitaa lake katika wimbo Asha, au Dada Lemmy. Charles Kazembe akiwa na Morogoro Jazz anakumbukwa katika upigaji wa rythm kwenye nyimbo kama Wajomba Wamechacha, yeye alifuata upangiliaji wa nyuzi za gitaa kama alivyokuwa anafanya Vata Mombasa wa Lipualipua, yaana kuweka nyuzi mbili zenye unene sawa katika gitaa lake, uzi namba 1 na namba 4. Hao ni wachache tu kulikoweko na wengi marufu, wote wakijitahidi kuwa na staili yao, Butiama Jazz ilikuwa tofauti na Western Jazz, au mipigo ya Mzee Chachil wa Urafiki. Kama nilivyosema hapo juu katika kipindi hiki huko Zaire kulikuwa na mipigo mbalimbali ya gitaa la rythm, ikiwemo kitu kipya kilichoanzishwa ambapo katika ufungaji wa nyuzi ,wapiga rythm wakauondoa uzi namba nne na kuweka uzi namba moja, hivyo kukawa na nyuzi namba moja 2 katika gitaa, hapo ndipo akina Vata Mombasa wakaweza kuleta utamu mpya katika upigaji wa rythm. Wakati huo Orchestra Kiam wakawa wanajivunia kupiga rythm kwa spidi kali sana,vibao kama Kamiki, Bomoto ni ushahidi wa kazi hizo. Utamu wa ufungaji wa nyuzi kwa staili hii uliweza kusikika vizuri katika gitaa lililopigwa mwanzo kabisa wa wimbo Andoya. Leo vionjo vya upigaji huo vinarudi kwa njia ya ajabu sana. Vikundi vya taarab vimeanza 'kuachia rythm' gitaa moja kubaki linapiga peke yake, japo wao hupiga gitaa la solo lakini staili ni ile ya enzi, na ukweli Taarab wameteka wapenzi wengi wa dansi. Ni ushauri utakaofaa kwa bendi zetu kurudisha hadhi ya gitaa hili katika bendi zao.

Comments