Maafisa Utamaduni unajua kuwa hawako chini ya Wizara ya Utamaduni?


Pamoja na maelezo mazuri ya Serikali kuwa inawajali wasanii, kuna maswali kadhaa ambayo yanajitokeza na kuleta maswali makubwa zaidi. Idara ya Utamaduni imekwisha hama Wizara zaidi ya kumi toka nchi hii ilipopata Uhuru, kwanini?,  Mwaka 1995 na pia mwaka 2010,Idara hii ilisahauliwa kutajwa wakati wa kutangaza Baraza la Mawaziri baada ya Uchaguzi Mkuu, mwaka 2010 tulipewa taarifa kuwa jambo hilo lilitokea kwa bahati mbaya mwaka 1995 hapakutolewa maelezo yoyote, ila kimya kimya ikaelezwa Utamaduni utaendelea kuwa chini ya Wizara ya Elimu.
Kuanzia kipindi cha miaka ya 90, Serikali ilifuta ngazi kadhaa za uongozi katika  Utamaduni, kulikuweko na nafasi ya Kamishna wa Utamaduni haiko tena, kulikuweko na nafasi ya  Afisa Utamaduni Mkoa, nayo haiko tena. Wako Maafisa Utamaduni wa Wilaya na Manispaa, lakini hawa sasa wako chini ya TAMISEMI, Wizara tofauti na ile inayohusika na Utamaduni. Haichukui akili kubwa kuona tatizo lililo wazi linatokea.
Nimeshawahi kumsikia Afisa Utamaduni mmoja Jijini Dar es Salaam akitamba kuwa yeye hababaishwi na Baraza la sanaa La Taifa, na ni kweli kwani hayuko chini ya Wizara ya Utamaduni.
Shughuli za pamoja za Kitaifa zilnazohusu Utamaduni ni ngumu kuzifanya sasa, Mashindano ya Kitaifa ya kazi za sanaa hayasikiki tena, pia hata shughuli zinazohusika na maslahi ya pamoja ya wasanii kama vile ulinzi wa haki za wasanii kwa mfano Hakimiliki umekuwa hobela hobela maana hakuna ajenda ya pamoja kwa viongozi hawa wanaotegemewa kuwa karibu kabisa na wasanii. Maafisa Utamaduni wa Wilaya wamekuwa zaidi ni wakusanyaji wa pato la Wilaya bila kuwa na mchango kwa wadau waliomo katika tasnia mbalimbali za Utamaduni wilayani mwao. Miaka ya nyuma sana Afisa Utamaduni alikuwa kimbilio la msanii, aliweza kutafuta vifaa vya muziki kwa wanamuziki, kutafuta maeneo ya kufanyia mazoezi kwa wasanii wasio na nafasi. Community Centers zilikuwa chini ya Afisa Utamaduni na kuwa mahala ambapo pako chini ya serikali na maalumu kwa shughuli za sanaa. Community Centers hazipo tena baada ya kugeuzwa aidha ofisi za Manisipaa au kukodishwa kwa watu binafsi kuongeza pato la serikali za mitaa bila kujali vijana waliomo katika Manispaa wanapewa sehemu maalumu kufanya shuguli zao za sanaa.
Ukiangalia Bajeti ya TAMISEMI  unajiuliza ni asilimia ngapi ya bajeti hiyo ilienda katika shughuli za Utamaduni? Utamaduni ukilelewa vizuri ni chombo chenye nafasi nyingi sana za ajira, huweza kuongeza pato la eneo husika kwa kuhamasisha maendeleo, kuleta uzalendo, ubunifu wa mambo mbalimbali ya Utamaduni huweza kuhamasisha Utalii katika Utamaduni, sehemu ya Utalii ambayo kwa bahati mbaya sana haijatumika kikamilifu katika kuongeza kipato cha nchi hii kwa ujumla.
Si ajabu siku hizi kusikia wasanii wakisema tutaenda kumuona Rais atusaide katika hili au lile, ni jambo la kusikitisha kuwa matatizo ya wasanii dawa mpaka kumuona Rais, wasanii wangapi wanaweza kupata nafasi hiyo katika nchi hii yenye watu milioni zaidi ya 40?
Ni muhimu kuangalia upya mfumo huu wa utawala katika nyanja ya Utamaduni

Comments