Historia ya muziki wa dansi Tanzania

Ukitaka kuongea muziki wa dansi uliingiaje nchini ni muhimu kujua historia ya mji wa Tanga. Tanga ndipo muziki wa dansi ulipoingilia nchini. Wajerumani waliusambaratisha mji wa Tanga kwa mizinga kati mwaka 1888 na 89. Na baada ya hapo kuujenga upya kwa kufuata mpangilio uliosababisha Tanga kuwa na mitaa maarufu kama barabara ya kwanza ya pili na kuendelea. Wajerumani walianzisha shule ya kwanza ya serikali Tanga 1892 na hapohapo wakanzisha bendi ya shule ya kwanza, pamoja na kuwa Wajerumani hawakutawala muda mrefu baada ya hapo lakini Waingereza waliiendeleza sana bendi hiyo iliyokuwa ikipiga aina mbalimbali za muziki wa kigeni. Dansi ilianza kwanza kama klabu ambapo watu walialikana kuja kucheza aina mbalimbali za muziki wa kizungu mtindo maarufu unaojulikana kama ballroom dancing. Aina hizi za klabu zilianzia Mombasa na kuingia nchini kupitia Tanga na kisha kuletwa Dar Es Salaam na klab iliyokuwa maarufu Tanga iliyoitwa Tanga Young Comrades Club, klabu nyingine ilianzishwa ikaitwa New Generation Club ambayo ilianzisha matawi miji mbalimbali. Klabu hizi ndizo zilizozaa bendi za dansi. Inaonekana Dar Es Salaam ndio ilikuwa ya kwanza kuwa na bendi yake African Association Jazz Band, ambapo wanamuziki wengine waliihama na kuanzisha Dar Es Salaam Jazz Band, hiki kilikuwa kipindi kati ya miaka 1930 na 1940, kwenye 1950 kulikuwa na bendi maarufu Bagamoyo iliyoitwa Lucky Star jazz band ambayo ilikuwa na urafiki na Dar Jazz. Baada ya hapo kulianza bendi ambazo wanamuziki na wanachama wake walipatikana kutokana na wanakotoka, kulikuweko na Ulanga Jazz band ya Wapogolo, Rufiji Jazz Band iliyoanzishwa na Wandengeleko, Western Jazz iliyoanzishwa kwanza na Wanyamwezi. Bendi zote hizi baadae zilikuja kuwa na wanachama mchanganyiko bila kujali uzawa. Na kulikuweko na Skokian Jazz Band hii ilikuwa ni bendi na klabu ya watu mchanganyiko. Mwaka 1958 wanamuziki kutoka Kilwa walianzisha Kilwa Jazz Band wanamuziki hawa walitoka bendi iliyoitwa Tanganyika Jazz. Ilipofika 1966 bendi ilikuwa na wanamuziki takribani 26, 15 wakiwa Kilwa A na 11 Kilwa B. Zamani bendi zilikuwa na mtindo wa kuwa na bendi B ambayo ni ya Vijana. Patrick Balisdya aliwahi kuwa Dar Jazz B. Kilwa Jazz ilikuwa na wanachama kama 50 wengine wakiwa viongozi wa juu serikalini. Waliolipa ada ya uanachama na hivyo kuweza kuingia madansi ya bendi bila kulipa. Wakati huo makao makuu ya Kilwa Jazz yalikuwa katika ukumbi ambao kwa sasa unaitwa Kwa Madobi maeneo yaa Jangwani

Comments